MADA: UFAHAMU UGONJWA WA MKANDA WA JESHI
Mkanda wa jeshi (shingles) ni jina linalotumika mitaani kuutaja ugonjwa unaoshambulia ngozi na kujenga tabaka la vijipele vikubwa venye majimaji ambavyo mara nyingi hukamata upande mmoja wa mwili. Ingawa vijipele vya mkanda wa jeshi vinaweza kutokea sehemu yo yote ya mwili, mara nyingi hupenda kuota kifuani, shingoni, usoni, mgongoni na mikononi. Vijipele hivi hukaa juu ya ngozi kwa muda wa wastani wa wiki mbili hadi sita kisha hupotea. Vipele vya mkanda wa jeshi huambatana na maumivu makali na kusikia ngozi kuwaka moto. Aghalab ugonjwa huu humrudia mtu zaidi ya mara moja.
Mkanda wa jeshi huwapata zaidi watu wenye umri mkubwa, zaidi ya miaka 50, utafiti ukionyesha kuwa zaidi ya nusu ya watu wenye umri wa zaidi ya miaka 80 hupatwa na mkanda wa jeshi. Vilevile huwapata zaidi watu waliopatwa na magonjwa yanayopunguza kinga za mwili, kama vile, UKIMWI na saratani. Tiba za mionzi na chemotherapy huweza kupunguza kinga za mwili za mgonjwa na kumfanya awe kwenye hatari kubwa ya kupata mkanda wa jeshi.